Askofu wa Kanisa la Ufufuo na Uzima, Josephat Gwajima amemwomba Rais 
Jakaya Kikwete kuvikemea vyombo vya dola vinavyomfuatafuata vikihoji 
mambo binafsi na kwamba akishindwa kufanya hivyo itakuwa wazi kwamba 
yeye ndiye anawatuma.
Akihubiri mamia ya waumini wa kanisa hilo jana, Gwajima alisema amekuwa 
akifuatwafuatwa na vyombo vya Serikali utadhani yeye si raia wakati ni 
Mtanzania halisi.
“Rais Kikwete tafadhali namuomba awakemee watu hawa… asipowakemea, basi 
kanisa langu litajua kwamba yeye ndiye anayewatuma,” alisema Gwajima 
huku akishangiliwa na waumini waliokuwa wakimsikiliza.
Huku wakinyeshewa na mvua, waumini hao walikuwa wakimsikiliza Askofu 
Gwajima, siku tatu baada ya kiongozi huyo kuhojiwa kwa mara ya pili na 
polisi na kutakiwa awasilishe mambo 10 yanayohusiana na usajili wa 
kanisa, uongozi na mali zake.
Uraia wake
“Mimi ni Mtanzania halisi acheni nifanye kazi ya Mungu, kama mnadhani 
mimi si Mtanzania, basi mmepotoka kwani kwa hilo mtashindwa,” alisema.
Alisema makundi ya jamii yamekuwa yakitoa kauli mbalimbali lakini hayabughudhiwi anavyofanyiwa.
“Madaktari, wanasiasa, wafanyabiashara wamekuwa wakitoa misimamo yao 
lakini hawabughudhiwi iweje Gwajima tu? Nitaendelea kuwapa vidonge vyenu
 kila mtakapopotoka, nafanya kazi ya bwana,” alisema.
Kuhusu utajiri wake
Gwajima alisema amekuwa akishangazwa na vyombo vya Serikali vinavyohoji 
utajiri alionao bila kujua anaongoza idadi gani ya waumini. Alisema 
anaongoza kanisa lenye waumini zaidi ya 70,000 ambao ni kama watoto wake
 na kwamba yeye ni baba yao wa kiroho.
“Waumini hawa mimi ni baba yao wa kiroho, nikiwaomba kila mmoja anipe 
Sh1,000 tu nitakuwa na Sh70 milioni, halafu mnahoji utajiri ninaupata 
wapi?” alisema na kisha kuwauliza waumini hao… “Hivi baba yenu 
nikiwaomba kila mmoja anipe Sh1,000 mtanipa au mtaninyima?”
Alijibiwa, “Tutakupaaaa!” Baada ya majibu hayo waumini hao walianza 
kupeleka fedha katika jukwaa kuu huku wakiimba nyimbo za kumtukuza 
Mungu.
