Waziri wa Kazi na Ajira Mhe. Gaudensia Kabaka amesoma Muswada wa Sheria 
ya Kuratibu Ajira za Wageni nchini wa mwaka 2014 kwa mara ya pili ikiwa 
muswada huu umelenga masuala mbalimbali ikiwemo mabadiliko ya kiuchumi 
pamoja na mahitaji ya kiteknolojia ambayo ni kichocheo kikubwa  cha 
uhamiaji wa nguvu kazi kutoka nchi moja kwenda nyingine.
Mhe.Kabaka alisema kwa sasa zipo mamlaka nyingi zinazotoa vibali vya 
ajira kwa wageni kwa kuzingatia sheria zinazosimamia maswala ya 
Uhamiaji, Uwekezaji, Elimu, Biashara na Wakimbizi, hivyo hali hii ya 
kuwepo na mamlaka nyingi zinachangia  kusababisha usumbufu kwa 
wawekezaji na kokosekana kwa uwajibikaji pamoja na kuwepo na 
udanganyifu.
“Kutungwa kwa sheria hii kunalenga kutelekeza kwa manufaa ya nchi yetu 
mikataba ya kikanda inayoruhusu uhamiaji huru wa nguvu kazi hususani 
inayohusu itifaki ya soko la pamoja la Jumuiya ya Afika Mashariki na 
Ushirikiano wa Jumuiya ya nchi za kusini mwa Afrika SADC” alisema Mhe. 
Kabaka.
Katika kutekeleza mikataba ya kikanda na kimataifa kuhusu uhamiaji na 
nguvu kazi, utaratibu wa kutoa vibali vya ajira kwa wageni umekuwa 
ukitumika ili kuhakikisha nguvu kazi ya wageni hao inaleta manufaa kwa 
maendeleo ya kiuchumi na kijamii, na pia katika kulinda ajira za 
wananchi.
Kwa upande wa Msemaji Mkuu wa kambi rasmi ya upinzani Mhe.Celina Paresso
 Mbuge wa Viti Maalum-CHADEMA aliishauri Wizara ya Kazi na Ajira 
kushirikiana na wizara mtambuka kama Wizara ya Viwanda na Biashara na 
Idara ya Uhamiaji, kufanya ukaguzi wa vibali vya ajira hasa katika 
maeneo ambayo raia wa kigeni wanafanya shughuri zao bila kuzingatia 
sheria za nchi.
“Tanzania tuna maliasili nyingi, lakini dunia ya leo na ijayo 
itatawaliwa na wenye maarifa, kwa maana ya sayansi, teknolojia, elimu na
 ujuzi” alisema Mhe. Paresso
“kuwa na maliasili peke yake haitoshi, hatuna budi tujinoe kwa elimu na 
ujuzi, na hasa elimu inayomuwezesha mtu aajirike au ajiajiri” aliongezea
 Mhe. Paresso
Endapo Mhe. Rais ataridhia, Sheria hii itaanza kutumika tarehe 1 Julai, 
2015. Kutungwa na kuanza kutumika kwa Sheria ya Ajira ya Wageni Nchini 
kutakuwa na matokea chanya ikiwema uratibu mzuri wa ajira za wageni 
nchini, kuongezeka kwa ajira za watanzania na kuongezeka kwa ujuzi kwa 
wafanyakazi wa Tanzania.
