Siku moja baada ya Katibu wa Itikadi na Uenezi wa Halmashauri Kuu (Nec) 
ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), Nape Nnauye, kusema Mbunge wa Monduli, 
Edward Lowassa, anaweza kupoteza sifa za kuwania urais kutokana na 
makundi ya jamii yanayomiminika nyumbani kwake kumshawishi awanie nafasi
 hiyo, Lowassa amemjibu na kusema hawezi kuzuia mafuriko kwa mikono.
Kadhalika, Lowassa amesema mambo ya Chama hayajadiliwi mtaani (kwenye 
vyombo vya habari), bali malalamiko yoyote yanapelekwa kwenye vikao 
halali vya CCM, yanajadiliwa na kutolewa uamuzi kwa mujibu wa kanuni na 
taratibu.
Hata hivyo, amewataka wafuasi wake pamoja na makundi mbalimbali ambayo 
yalikuwa yamejiandaa kwenda nyumbani kwake kumshawishi, wasitishe kwanza
 safari yao hadi hapo Chama kitakapotoa maelekezo ya ‘namna ya 
kushawishi.’
Lowassa aliyasema hayo nyumbani kwake jana, alipokuwa akipokea ujumbe wa
 waendesha bodaboda 60 kutoka Wilaya ya Mbarali, mkoani Mbeya ambao 
walikwenda kumshawishi awanie urais muda utakapofika.
Alisema kwa kanuni na taratibu za CCM, mambo ya chama humalizwa kwenye 
vikao vya chama, kwa kuzungumza hadi kuelewana na kufikia muafaka, 
lakini siyo kwenye vyombo vya habari.
“Mambo ya Chama hayawezi kuzungumzwa kwenye vyombo vya habari kwenye tv,
 redio; mara huyu hivi, huyu hivi, mkiona chama kinakwenda kwenye 
utaratibu huo ni hatari sana…CCM ninayoijua mimi ni ya vikao, kwa hiyo 
sikusudii kujibu hizo hoja, kwanza rafiki yangu Bashe (Hussein), 
amezieleza vizuri sana, lakini sikusudii kusema zaidi ya hayo 
yaliyosemwa na Bashe,” alisema.
Alisema anashangaa kuona watu wakizusha kwamba watu wanaokuja nyumbani 
kwake kumshawishi amewaita na kuwalipa jambo ambalo ni uongo kwa kuwa 
hana fedha za kulipa watu wengi wanaokuja kwake na hana pia uwezo wa 
kuwapikia chakula.
“Wanasema mnakuja nimewaiteni ninawapa fedha, hela za kuwapa ninazitoa 
wapi, mkija hapa nikiwawekea maturubai ni kosa, mkiwa na viti ni makosa 
na wanasema nawapikieni chakula. Mambo ya ajabu sana, yanasemwa na watu 
wazima watu wenye heshima zao; juzi kulikuwa na vijana 300 hapa, 
nitawapikia chakula nitaweza wapi, ni vibaya sana kumdhalilisha mwenzako
 kwamba maisha yake yote akili yake ni kufikiria tumbo, huyu hana cha 
kufikiri isipokuwa tumbo,” alisema Lowassa.
“Nimewahi kuja huko Mbarali kuwashawishi mje kwangu? Au nimewapeni   
hela   leo   mlipokuja hapa, hata soda zenyewe hamjanywa,” alisema 
Lowassa huku vijana wakisema hawajashawishiwa naye.
Aliongeza: “Yananisikitisha sana maneno hayo, lakini hayanikatishi tamaa
 nitaendelea kama ilivyo kawaida. Nawahakikishie nimeyasikia maneno 
hayo, lakini najua maneno mazuri huwa yanazungumzwa kwenye chama, 
nategemea yatajadiliwa kwenye vikao vya chama.”
Lowassa alisema: “Na utaratibu huu ulioanza na watu, (kuja nyumbani 
kwake), mimi ni vigumu kuuzuia. Mimi ni vigumu kuzuia mafuriko kwa 
mikono. Mafuriko yanakuja mimi nayazuia kwa mikono, nitaweza kweli?”
“Ila nashauri tufanye hivi, wengine ambao hawajaja wanisikilize, hebu 
tusubiri Chama kitoe maelekezo, kama wamesema hii inatafsiriwa kwamba ni
 kampeni, tungoje basi wasema tufanye nini watu wanaotaka kuja 
kushawishi,” alisema.
Alisema watu wanaokwenda kumshawishi wanatii maelekezo yaliyotolewa na 
Mwenyekiti wa CCM Taifa, Rais Jakaya Kikwete, ambayo aliyatoa mjini 
Songea wakati wa sherehe za miaka 38 ya CCM, aliposema kwamba wanachama 
wanaweza kumshawishi mgombea wanayeona anafaa.
“Na mimi nilikuwapo kiwanjani pale akasema mkiona hao waliopo hawatoshi,
 bado muda upo washawishini wengine waingie. Sasa mkifanya hivi ni kosa,
 ni kampeni, ipi ni kampeni na ipi siyo kampeni?,” alisema na kuhoji.
“Kwa hiyo nawashauri wale ambao hawajaja, tusiingize mgogoro kwenye 
Chama, tungoje tupate maelekezo, mimi ninahakika tutapata nafasi, jambo 
moja ninahakika na ninataka kuwapa matumaini ipo siku Watanzania 
watapata uhuru wa kusema juu ya mtu mimi, iko siku watapiga kura zao 
kusema naam ama hapana kwa hiyo tungojee hiyo siku.”
Alisema anatambua Watanzania wengi wanampenda kwa kazi zake alizofanya 
akiwa kwenye ngazi mbalimbali serikalini na kutaka wanaomshambulia 
wasubiri Watanzania wenyewe waamue kwenye sanduku la kura.
“Ninahakika wapo Watanzania wengi wanaonipenda kama walivyosema kwa kazi
 zangu, watapata nafasi ya kusema naam ama hapana, kwa hiyo huyo 
anayepiga kelele nyingi sijui nitoke kwenye chama sijui nifanye kitu 
gani angoje wanaCCM na Watanzania waamue. Mimi ni mwanademokrasia 
naamini kwenye demokrasi, lakini naamini kwenye utendaji bora, kama 
mlioufanya leo wa kutembea kilometa 600 kutoka Mbarali kuja kunitembelea
 hapa ni kazi kubwa ya utashi mkubwa sana, ni watu wanaojitolea, 
wanaojiamini, na mimi ninaamini Watanzania wengi wanaoniamini kwa mambo 
ambayo nimeyafanya,” alisema.
Aliwasihi vijana hao kupuuza taarifa zilizotolewa kwenye vyombo vya 
habari jana na kuwaomba waendelee kukiunga mkono chama hicho.
Alisema safari ya vijana hao kusafiri kilimita 600 kwa bodaboda kutoka 
Mbarali imemtia moyo na haya kwa kuweka wazi mambo wanayoyaamini.
Alisema vijana wa bodaboda wanafanya kazi kubwa nchini ikiwamo ulinzi na
 usalama hivyo ni kundi linalohitaji kuendelea kusaidiwa.
“Mimi nitaendelea kushirikiana nao siku zote katika nafasi yoyote 
nitakayokuwa nayo. Mmekuja siku mbaya kidogo kwa sababu jana kuna watu 
wamesema kwenye vyombo vya habari maneno mengi ambayo kwa malezi yangu 
mimi mambo ya chama humalizwa kwenye vikao siyo kwenye vyombo vya 
habari, lakini yasiwakatishe tama,” alisema.
Awali, Kamanda wa Vijana wa CCM wilayani Mbarali, Ibrahim Mwakabwanga, 
alisema Lowassa hana uwezo wa kushawishi kila kundi na hata wao 
wamejikusanya wenyewe, wamejigharimia na wameacha shughuli zao na kuamua
 kuja Dodoma kumshawishi kwa kuwa wanaona ndiye kiongozi ndani ya CCM 
anayefaa kwa sasa.
